Home » » Reginald Mengi Atunukiwa Tuzo ya Mafanikio ya Maisha..!!

Reginald Mengi Atunukiwa Tuzo ya Mafanikio ya Maisha..!!

MWENYEKITI wa IPP , Reginald Mengi, ametunukiwa Tuzo ya Mafanikio ya Maisha katika Kusaidia Jamii kwa mwaka 2013 katika eneo la ukanda wa nchi za Afrika Mashariki.
Tuzo hiyo ijulikanayo kama East Africa Philanthropy Awards 2013, inatolewa na Shirikisho la Taasisi Zinazofadhili Maendeleo ya Jamii katika Afrika Mashariki (EAAG) lenye makao yake makuu nchini Kenya. Tuzo hiyo alikabidhiwa na Balozi wa Norway Nchini, Ingunn Klepsvik katika hafla iliyofanyika juzi usiku jijini Dar es Salaam.

Mtendaji Mkuu wa EAAG, Nicar Sabula alisema shirika lao lilianzishwa mwaka 2003 na linaunganishwa na mashirika yanayofadhili maendeleo ya jamii katika Ukanda huu wa Afrika Mashariki.
Akizungumzia tuzo hiyo, alisema ilizinduliwa mwaka 2011 huko Arusha wakati wa mkutano mkuu wa shirika hilo.
Alisema tuzo hiyo inalenga kuwatambua, kuwathamini kampuni, mashirika au watu wa aina mbalimbali, ambao wamekuwa wanatoa misaada kwa jamii katika eneo la Afrika Mashariki.

"Ni tuzo kwa watu ambao wametoa muda, fedha, taarifa bidhaa na huduma na sauti zao zikasaidia kuboresha maisha au kundi fulani la watu," alisema Sabula.
Aliongeza kuwa ili mtu au shirika liweze kuwa na sifa za kupewa tuzo hiyo ni lazima hatua yake ya msaada, iwe ya viwango vya juu ambayo inaweza kuwavutia wengine.
Tuzo hiyo ilizinduliwa mwaka jana huko Entebe nchini Uganda, ikiwa ni miongoni mwa tuzo nane zinazotolewa na asasi hiyo.

Alisema jumla ya watu 60 walipendekezwa kupewa tuzo hiyo kwa mwaka huu kutoka nchi zote za Afrika Mashariki. Kati ya hao, watu 15 walipenya katika mchujo wa awali, ambao ulifanywa na watu mashuhuri kutoka katika asasi zisizo za kiserikali.
"Kati ya hao, watu wanane walikidhi vigezo vya kupewa tuzo hizo na Mengi akiwa ni mmojawapo ya watu ambao walishinda Tuzo ya Mafanikio ya Maisha katika kusaidia jamii (Lifetime Achievement in Philanthropy Award).

Mwenyekiti wa EAAG, Tom Were alisema Afrika Mashariki ili isiendelee kutegemea misaada kutoka nje ya bara hili, inategemea kuzalisha akina Mengi wengi ili waweze kujitokeza kusaidia jamii inayowazunguka.

Alimwelezea Mengi kuwa ni mtu ambaye amejitoa katika maeneo mengi kusaidia jamii na kupata mafanikio, ndio maana amechaguliwa kutunukiwa tuzo hiyo.


 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BONGONEWS TZ - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger