Home » » HUYU NDIYE WINTA WA JUMBA LA DHAHABU ALIYENUSURIKA KUUWAWA KWA RISASI

HUYU NDIYE WINTA WA JUMBA LA DHAHABU ALIYENUSURIKA KUUWAWA KWA RISASI

 LICHA ya kipaji cha kuzaliwa alichoanza kukionyesha tangu akiwa kinda wakati akisoma Shule ya Msingi Mgulani, msanii Angel John Komba 'Winta' anakiri kuwapenda na kuvutiwa kupita kiasi na Genevieve Nnaji wa Nigeria na Yvonne Cherly 'Monalisa' kulichangia kuingia kwake katika fani ya uigizaji.
Winta, mmoja wa waigizaji wa kike mahiri nchini aliyetamba na kazi mbalimbali kama tamthilia na filamu anasema nyota hao walikuwa wakimkosha kila alipoziona kazi zao na kuapa kuwa ni lazima na yeye aje kuwa staa kama wao.

"Nnaji na Monalisa ndiyo walinipa mzuka wa kujibidiisha katika sanaa ya uigizaji kwani walinikosha na mpaka sasa navutiwa nao," anasema.
Anasema kabla ya kuvutiwa na umahiri wa wanadada hao alikuwa amejikita kwenye sanaa ya kupiga na kucheza ngoma enzi akiwa darasa la sita na kuendelea hata alipojiunga na Sakhafa Sekondari ambapo tayari alishaanza kuigiza.
Hata hivyo anasema kujitosa kwake rasmi katika uigizaji, ilikuwa mwaka 2001 alipokutana na Jumanne Kihangale 'Mr Chuz' anayemtaja kama mmoja wa watu asiyoweza kuwasahau kwa alivyomsaidia kufika mahali alipo sasa na kuwa miongoni mwa waasisi wa kundi maarufu ya uigizaji la Fukuto Arts Professional.
"Kiukweli nilitumbukia rasmi kwenye uigizaji mwaka 2001 nikiwa miongoni mwa waasisi wa kundi la Fukuto na kazi ya kwanza kuicheza ilikuwa ni igizo lililokimbiza nchini la Jumba la Dhahabu na mingine iliyokuja baadaye kabla ya kuhamia kwenye filamu kwa kucheza kazi mbalimbali zilizonipaisha ndani na nje ya nchi," anasema.
Mrembo huyo anayeishabiki Simba na mabingwa watetezi wa England klabu ya  Manchester United, anasema tangu ameingia kwenye fani hiyo anashukuru amepata mafanikio mengi ya kujivunia baadhi hapendi yaanikwe gazetini.
Winta anadai mbali na manufaa ya kiuchumi, sanaa imemfanya afahamiane na watu wengi na kupata rafiki na kutembea sehemu mbalimbali.
"Nashukuru sanaa imenisaidia kwa mambo mengi ya kujivunia, japo sijaridhika kwa vile ndoto zangu ni kuja kumiliki kampuni binafsi itakayozalisha na kusambaza kazi zangu na za wasanii wenzangu," anasema.

MKASA
Kisura huyo anayependa kula ugali kwa mlenda na dagaa mchele wa kukaangwa, anasema sanaa ya Tanzania imezidi kupiga hatua kubwa kulinganisha na siku za nyuma japo anadai wizi na unyonyaji unawafanya wasanii washindwe kunufaika.
Anasema, lazima serikali na mamlaka zinazosimamia fani hiyo kutoa makucha yake ili kuwabana wanyonyaji na wezi wa kazi za wasanii ili kuinua maisha ya wasanii tofauti na sasa wengi wao wakiishi maskini tofauti na jasho lao.
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgTRDk6Q3zQ4vg5D6bwHJWbpwzKVJOXh552k4MjNNR1JaF9i57-g7-nURb4Td1F_k-diJsqz3yLCuc_JMiykwD4KCZoUx25CqnZGJHlAMga9xSQsZ6RIKt60XSkT1eNPNqn7x1p5frlqYE/s400/winterwebMsanii Winta katika pozi

 Pia anataka watengeneze miundo mbinu itakayowasaidia chipukizi kuendeleza vipaji vyao ili kusaidia kuondoa tatizo la ajira sambamba na serikali kuvuna pato kupitia fani hiyo.
Juu ya tukio la furaha, Winta anasema ni siku alipojaliwa kujifungua mtoto wa kiume aliyenaye, huku akidai hawezi kuusahau mkasa uliowahi kumkuta hivi karibuni alipokuwa na rafikize 'wakila bata' na kubadilishana mawazo baa.
Anasema akiwa na wenzake hawana hili wala lile, ghafla Pub waliyokuwepo (jina limehifadhiwa) ilivamiwa na majambazi ambao waliwamrisha wateja wote kulala na yeye kwa ubishi alikurupuka ili kukimbia na kufyatuliwa risasi iliyomkosakosa sentimita chache na kwa kiwewe alijikuta akitumbukia kwenye mtaro wa maji machafu yaliyochanganyika na kinyesi.
Winta anasema kila anapolikumbuka tukio hilo la kusalimika kufa kwa risasi na jinsi alivyokoga uchafu huo hukosa raha.
"Siwezi kulisahau tukio hilo kwa jinsi nilivyonusurika kifo cha risasi na kutumbukia kwenye mtaro wa kinyesi, yaani ilikuwa balaa. Ila nashukuru  Mungu aliinusuru roho yangu," anasema.
Winta ambaye hajaolewa japo ana mtoto mmoja, anasema hakuna msanii wa kiume anayemkuna nchini kama mkongwe Amri Athuman maarufu kama Mzee Majuto.
"Huyu mzee noma, hana mpinzani na anajua kitu anachokifanya katika fani," anasema mwanadada huyo anayejikubali mwenyewe kwa uwezo alionao.

ALIPOTOKAAngel John Komba 'Winta' alizaliwa mwaka 1982 katika hospitali ya Temeke, Dar es Salaam kabla ya kuanza Shule ya Msingi Mgulani kabla ya kujiunga na Sakhafa Sekondari ambapo tayari alishaanza kujishughulisha na sanaa akicheza, kupiga ngoma na kuigiza.
Winta anayependa kunywa Fanta Passion na Castle Light, baada ya kumaliza shule alitumbukia rasmi kwenye sanaa hiyo akianzia kundi la Fukuto Arts Professional na kutamba nalo na tamthilia kadhaa kabla ya kuangukia kwenye filamu.
Baadhi ya filamu alizoigiza mwanadada huyo anayependa kutumia muda wa ziada kuangalia 'muvi' kuchati na kusoma vitabu na magazeti ni pamoja na 'Shock' aliyoigiza na marehemu Steven Kanumba, 'I Hate My Birthday', 'Pigo la Yatima', 'Kovu la Laana' na nyingine.

Winta akiwa na marehemu Kanumba walipokuwa wakiigiza filamu ya The Shock
Winta anayewataka wasanii wenzake kutegemea vipaji walivyonavyo na kuvitumikia kwa ufanisi badala ya kujihusisha na skendo au vitendo vya ushirikiana.
"Hakuna siri kwa sasa wasanii wanaendekeza sana mambo ya kishirikiana kwa kushinda kupishana kwa waganga ili kuroga na kutembelea nyota za wenzao, ila ukweli mtu anayejiamini na kutegemea kipaji hawezi kufanya upuuzi huo ambao hausaidii zaidi ya kujidhalilisha," anasema.
Mwanadada huyo anayemshukuru mno Mr Chuz na watu wengine waliomsaidia kwa namna moja au nyingine kufika alipo, anaiomba jamii iwachukulie wasanii kama watu wengine na pale wanapokosea wasiwahukumu wote au kuwaona watu wa ajabu kwa sababu hakuna binadamu aliyekamilika.
"Pia watuunge mkono kwa kununua kazi zetu sambamba na kutusaidia kupambana na maharamia kwa kuacha kununua kazi feki badala yake wazinunue kazi halisi ili tuweze kuendelea kuwapa burudani," anasema.


 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BONGONEWS TZ - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger