Home » » SIMANZI...!! AUAWA NA KUTUPWA SHAMBANI, MWINGINE ACHOMEWA NYUMBA..AFIA NDANI...

SIMANZI...!! AUAWA NA KUTUPWA SHAMBANI, MWINGINE ACHOMEWA NYUMBA..AFIA NDANI...

Oktoba 16, mwaka huu, majira ya saa saa nne na nusu usiku, huko katika Kijiji cha Mahenje Kata ya Myovizi, Tarafa ya Iyula wilayani Mbozi mkoani hapa, mtu mmoja asiyefahamika jina wala makazi, jinsi ya kiume, umri kati ya miaka 20-25, alikutwa ameuawa na watu wasiojulikana na mwili wake kutupwa shambani.
Wakati mwili huo umehifadhiwa katika hospitali ya wilaya ya Mbozi, polisi wameanza uchunguzi wao ili kubaini chanzo cha mauaji hayo ambayo marehemu alikutwa na jeraha upande wa kulia wa ubavu wake.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Kamishna Msaidizi Diwani Athuman alithibitisha kutokea kwa tukio hilo huku akitoa wito kwa ye yote mwenye taarifa juu ya mtu au watu waliohusika katika tukio hilo kuzitoa katika mamlaka husika ili wakamatwe na sheria ichukue mkondo wake.
Katika tukio lingine, siku hiyo hiyo, katika Kijiji cha Isalalo, Kata ya Msia, Tarafa ya Igamba wilayani Mbozi, Tusamale Wilega (70) ambaye ni mkulima, alifariki dunia akiwa amelala ndani ya nyumba yake baada ya mtu au watu wasiofahamika kuchoma moto nyumba yake.
Ilielezwa kuwa marehemu alikuwa anaishi peke yake katika nyumba hiyo iliyojengwa kwa matofali mabichi na kuezekwa kwa nyasi.
Bado polisi wanaendelea kuchunguza chanzo cha moto huo.
Mwili wa marehemu umefanyiwa uchunguzi na kukabidhiwa ndugu kwa mazishi.
Kamanda Athumani alithibitisha kutokea kwa tukio hilo huku akitoa wito kwa mtu au watu wenye taarifa kutoa ushirikiano kwa polisi.
-GPL
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BONGONEWS TZ - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger