Home » , » "Siyo vibaya kwa wanaotaka kuwania urais kutangaza nia mapema, kwa sababu inawapa nafasi wananchi kuwapima"....Hii ni kauli ya January Makamba baada ya kuhojiwa na kamati ya maadili jana

"Siyo vibaya kwa wanaotaka kuwania urais kutangaza nia mapema, kwa sababu inawapa nafasi wananchi kuwapima"....Hii ni kauli ya January Makamba baada ya kuhojiwa na kamati ya maadili jana



Kamati ndogo ya Maadili ya CCM imeendelea kuwahoji wanachama wake walioonyesha nia ya kuwania urais, jana ilikuwa zamu ya mawaziri watatu. 
 
Waliotarajiwa  kuhojiwa jana ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba.

 Makamba alikuwa wa kwanza kufika mbele ya kamati hiyo jana asubuhi, huku Wassira akifuatia. Hata hivyo, Membe hakuonekana.
 
Hata hivyo, kanuni za uongozi wa maadili za CCM kifungu cha 7 (i) kinaeleza kuwa wanachama wenye nia ya kugombea nafasi za uongozi katika muhula unaofuata, yaani ubunge, uwakilishi, udiwani na nafasi nyingine katika chama wanaweza kutangaza nia zao, lakini hawaruhusiwi kufanya kampeni kabla ya muda uliowekwa rasmi, muda wa kampeni unaanza baada ya majina ya wagombea kuteuliwa na kikao kinachohusika.
 
Makamba
Baada ya kuhojiwa Makamba, alisema siyo vibaya kwa wanaotaka kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kutangaza nia mapema, kwa sababu inawapa nafasi wananchi kuwapima.
 
Mbali na hilo Makamba alisema siyo dhambi kwa mtu kuonyesha nia, bali ni dhambi kwa mtu kutoa fedha kwa nia ya kutaka uongozi na kuvitaka vyombo vya dola kuchukua hatua za kisheria kwa watu wa aina hiyo.
 
Kikao hicho kinachoongozwa na Makamu Mwenyekiti Bara, Philip Mangula, juzi kiliwahoji mawaziri wakuu wa zamani Edward Lowassa na Fredrick Sumaye pamoja na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja, ambaye pia aliwahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini.
 
“Ipo faida ya kuwajua mapema wanaotaka uongozi kuliko kuwajua mwishoni, kwa sababu mnapata faida ya kuwachambua na kuwauliza maswali, mbaya ni mtu kutoa pesa ama kutumia pesa.
 
“Hata katika maoni yangu na ushauri (ndani ya kikao hicho cha maadili), nimesema kwamba hilo ndilo kubwa na la msingi, kwa sababu linawaweka pembeni watu wenye vipaji vya uongozi kama huna fedha basi huwezi kuwa kiongozi,” alisema Makamba.
 
Alisisitiza matumizi ya fedha katika kutafuta uongozi yanakatazwa kwa mujibu wa kanuni za chama chao na sheria za nchi na kwamba ushahidi unapopatikana chama kifanye kazi yake na Serikali ichukue hatua dhidi yao.
 
Makamba alisema ipo sheria ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na Sheria ya Gharama za Uchaguzi, ambazo zote zinakataza matumizi ya fedha.
 
“Kwa hiyo hawa wanaotajwa wanatumia fedha vilevile vyombo vya dola viwachukulie hatua, siyo tu kwenye chama,” alisema Makamba.

Makamba alisema kuwa mazungumzo yao ndani ya kikao hicho yalikwenda vizuri, akidai yeye hakuitwa kwa ajili ya kugawa fedha kwa wananchi na wala hakukuwa na shitaka lolote, isipokuwa ilikuwa ni kutoa ushauri na kukumbushana kuhusiana na misingi muhimu ya chama chao ya namna ya kupata uongozi.
 
“Kwa hiyo nilipata fursa nzuri ya mimi kutoa ushauri wangu kuhusiana na namna ambavyo tunaweza kuyafanya mambo haya vizuri zaidi, na namna ambayo tunaweza kutafuta uongozi kwa namna nzuri zaidi badala ya kukigawa,”alisema.
 
Makamba alisema kuwa mazungumzo yao yalikuwa mazuri sana na kwamba hakukuwa na jambo baya, wala hakuwa ameshitakiwa bali walikuwa katika majadiliano ya kawaida ya ndani ya chama na kuwa aliitwa kutokana na kutajwatajwa na wanachama.
 
Wassira
Kwa upande wake Wassira alisema hana mpango wa kutangaza kugombea urais leo wala kesho, lakini muda ukifika ataamua.
 
Alisema: “Kutamani nafasi ya urais siyo dhambi.”
Wassira alisema yeye ni mjumbe wa Kamati Kuu ya chama hawezi kutoboa mtumbwi ndani ya chama, halafu waangamie wote.
 
Alisema hajafanya vurugu zozote ndania ya chama na kwamba katika kikao cha jana aliitwa kwa ajili ya kujitathimini na kuangalia mustakbali wa chama katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
 
Ripoti ya kamati hiyo ya maadili ya chama huenda ikawasilishwa kwenye mkutano Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), unaotarajiwa kufanyika leo mjini Dodoma.
 
Akizungumzia suala hilo mwishoni mwa wiki iliyopita, Makamu Mwenyekiti wa CCM (Tanzania Bara), Philip Mangula alisema mwanachama yeyote wa chama hicho hatakiwi kutoa michango, misaada, zawadi kwa mtu au katika shughuli yoyote bila kupata ridhaa ya uongozi.
 
“Kufanya jambo hilo ni kwenda kinyume na kanuni za chama. Ndani ya chama kila ngazi ina Kamati ya Maadili, wote ambao wameanza kwenda kinyume na kanuni za chama watahojiwa katika kamati hizo,” alisema Mangula na kuongeza:
 
“Hairuhusiwi kuwasafirisha wajumbe, kuwapa malazi, chakula, vinywaji na ukifanya hivyo utakuwa unakwenda kinyume na utaratibu uliowekwa na Kamati ya Sheria, Katiba na Kampeni.”

Akihutubia kilele cha maadhimisho ya miaka 37 tangu kuzaliwa kwa chama hicho, Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete aliziagiza Kamati za Maadili na Usalama, kuwachukulia hatua stahiki viongozi na wanachama wake wanaomwaga fedha ili kupata uongozi.
 
Kadhalika, Rais Kikwete alipozungumza na wajumbe wa Halmashauri ya CCM ya Mkoa wa Mbeya, alisema kuanza kwa kampeni kabla ya wakati wake ni moja ya mambo yanayosikitisha na kwamba suala hilo limekabidhiwa kwa Mangula kwa hatua zaidi za kinidhamu.

>>Gazeti  la Mwananchi.
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BONGONEWS TZ - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger