WANAKWAYA sita wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mt. Kalory Rwanga, Usa River, mkoani hapa, wamelazwa katika Hospitali ya Misheni na ya Tengeru, Arumeru baada ya kujeruhiwa kwa bomu.
Walikutwa
na masahibu hayo juzi muda mfupi baada ya kutoka kanisani kwenye Mkesha
wa Mwaka Mpya saa 6.30 usiku, meta 100 kutoka Kanisa hilo, eneo la
Kisangani.
Mganga
Msaidizi wa hospitali hiyo, iliyoko chini ya Kanisa Katoliki, Fredrick
Mathew, alithibitisha jana kupokewa majeruhi watano, huku wawili wakiwa
na hali mbaya na wengine wakiendelea vizuri.
Alitaja
majeruhi hao kuwa ni Theresia Lesitare (33), Philipo Ambrose (22),
Alphonce Nyigo (19), Mary Merikiory (40) na Anna Mathew (19) wote wakazi
wa Lake Tatu, Usa River.
Majeruhi
mwingine ambaye hali yake si nzuri, Annet Baltazar (16) amelazwa katika
Hospitali ya Tengeru. Alisema majeruhi hao waliumia miguuni kwa
kuchanwa na mlipuko huo na baadhi ya vipande vya bomu, vilitolewa kwenye
miili yao na baadhi yao kushonwa kwa nyuzi kadhaa.
Kamanda
wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alithibitisha kupata
taarifa za tukio hilo na kueleza, kwamba uchunguzi wa tukio umeanza mara
moja na atatoa taarifa ukikamilika.
Akizungumza
na mwandishi wa habari hizi jana, Merikiory, alisema baada ya kutoka
kanisani akiwa na wanakwaya wenzake, waliondoka kuelekea nyumbani, Lake
Tatu.
Alisema
wakiwa barabarani, waliona gari aina ya Toyota Land Cruiser likienda
kwa kasi na lilipowakaribia, walisikia mlipuko na wakajikuta wamelala
kando ya barabara huku baadhi yao wakivuja damu miguuni na tumboni.
Aliongeza
kuwa gari hilo, halikusimama na lilipofika mbele waliokuwamo walifyatua
mabomu ya kutoa machozi, kutawanya makundi ya watu mbalimbali waliokuwa
wakionekana barabarani.
Alisema
waliomba msaada kwa Paroko wa Kanisa hilo, Patrick Njau, ambaye alitoa
gari na kuwapeleka Hospitali ya Misheni na wengine wakipelekwa Hospitali
ya Wilaya ya Tengeru kwa matibabu zaidi.
Askofu alia
Akizungumza
huku akitokwa machozi baada ya kutembelea majeruhi, Askofu Mkuu wa
Jimbo Kuu Katoliki la Arusha, Josephat Lebulu alisema ameshangazwa na
tukio hilo. Alisisitiza kuwa Kanisa Katoliki, limechoka kuandamwa na
matukio ya aina hiyo.
“Waumini
wanakosa gani hadi watupiwe bomu, kwa nini polisi wako kimya hadi leo
wasiseme? Kuna siri gani? Kwa nini kila siku ni Wakatoliki tu ndio
wanapigwa mabomu, tunataka haki itendeke, watu wametoka kanisani usiku,
wamekosa nini? Usalama uko wapi?” Alihoji.
Aliendelea:
“Tumekosa nini, kupigwa mabomu kila siku hapa Arusha? Tumeshuhudia
Olasiti, tukashuhudia Soweto sasa ni hapa Usa,” alisema. “Na kwa hili
Kanisa hatutakubali hata kidogo, tunataka wahusika wawajibishwe na
walioficha uovu huu wawajibishwe la sivyo viongozi walioficha uovu huu
wawajibishwe, Mungu atasimama kwa ajili yetu,” alisema.
Mei
mwaka jana, bomu lililorushwa liliua watu watatu na kujeruhi wengine
zaidi ya 60 kwenye Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi
Parokia ya Olasiti, mjini Arusha.
Waumini
walikuwa wamejumuika katika misa ya uzinduzi wa Kanisa hilo. Misa hiyo
ilikuwa ikiongozwa na Balozi wa Vatican nchini na Mwakilishi wa Papa
Francis, Askofu Francisco Padila kwa kushirikiana na Askofu Lebulu.
>>Habari leo
>>Habari leo