Afrika
na dunia inatarajiwa kushuhudia kitu kipya katika maziko ya Rais wa
zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela (95) aliyefariki dunia juzi,
baada ya kuugua kwa zaidi ya miezi sita.
Serikali
ya Afrika Kusini imesema kiongozi huyo ambaye atazikwa Desemba 15,
imeandaa mazishi ya kihistoria yanayosemekana yatazidi yale ya Papa John
11.
Matukio
ya shughuli mbalimbali zinazohusu mipango ya maziko ya kiongozi huyo
maarufu yanatarajiwa kushuhudiwa sehemu mbalimbali duniani, tofauti na
tukio jingine lililowahi kutokea barani Afrika mbali na kombe la dunia.
Rais
Jacob Zuma alisema jana kwamba “Mpendwa wetu Madiba atazikwa kwa heshima
zote za Serikali. Nimeagiza bendera zote za Afrika Kusini zipepee nusu
mlingoti na hiyo itaendelea hivyo hadi tutakapokamilisha mazishi yake.
Mazishi
ya Mandela yanalinganishwa na yale ya Papa John Paul II mwaka 2005,
ambayo yalihudhuriwa na wafalme watano, malkia sita wa falme mbalimbali
na marais wapatao 70 na mawaziri kadhaa, wakiwamo wafuasi wake zaidi ya
milioni mbili. Yanakadiriwa pia kulingana na maziko ya Winston Churchil
aliyekuwa Waziri Mkuu wa Uingereza mwaka 1965.
Marais
wote wa Marekani walio hai wanatarajiwa kuhudhuria mazishi hayo iwapo
afya zao zitawaruhusu kusafiri, pamoja na Prince Charles wa Uingereza na
hata Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe. Pia watu maarufu wenye urafiki wa
karibu na Mandela akiwamo msanii Oprah Winfrey wameshathibitisha
kuhudhuria.
Changamoto la kiusalama
Kutokana
na idadi kubwa ya wakuu wa nchi na watu maarufu duniani wanaotarajiwa
kufika Afrika Kusini, suala la usalama limeelezewa kuwa changamoto mpya
kwa vyombo vya usalama nchini humo.
Afrika
Kusini imekuwa moja ya nchi zinazokabiliwa na matukio ya uporaji na
mauaji yanayotokana na idadi kubwa ya wahalifu, wengi wao wakidaiwa kuwa
wahamiaji haramu.
“Huyu
ni shujaa wa dunia. Tutafanya mipango ya mazishi makubwa ambayo
hayajawahi kushuhudiwa. Nadhani kila nchi itakuwa imeandaa utaratibu
wake wa namna ya kushiriki,” alisema mmoja wa wanadiplomasia wa Afrika
Kusini ambaye hakutaka kutajwa jina lake.
Siku 11 za maombolezo
Serikali
ya Afrika Kusini, kwa mujibu wa gazeti la The Guardian tayari imeweka
wazi ratiba ya siku 11 za maombolezo tangu alipofariki dunia juzi jioni.
Japokuwa ratiba hiyo ilishaandaliwa karibu mwaka mmoja uliopita na
kupitiwa na kufanyiwa maboresho katika baadhi ya maeneo, inaonyesha
namna maofisa wa Serikali ya Afrika Kusini walivyolipa uzito suala hilo
na kulifanya kuwa tukio la kukumbukwa katika historia.