Home » » HATIMAYE...! AZAM YAPAA MPAKA NAFASI YA PILI IKIIONDOA YANGA KATIKA MSIMAMO WA LIGI KUU BAADA YA KUISAMBARATISHA MGAMBO JKT

HATIMAYE...! AZAM YAPAA MPAKA NAFASI YA PILI IKIIONDOA YANGA KATIKA MSIMAMO WA LIGI KUU BAADA YA KUISAMBARATISHA MGAMBO JKT

AZAM FC imepaa hadi nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, kufuatia ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mgambo JKT ya Tanga jioni ya leo Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam. Ushindi huo, unaifanya timu hiyo ya bilionea Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa itimize pointi 14, baada ya kucheza mechi nane, ikiwa sasa inazidiwa pointi moja tu na Simba SC iliyo kileleni, japokuwa Azam imecheza mechi moja zaidi. Yanga SC yenye pointi 12 inaangukia nafasi ya tatu.


Ushindi wa leo umetokana na mabao ya winga kinda aliyepandishwa kutoka kikosi cha pili, Farid Malik dakika ya 66 na mfungaji bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, Kipre Herman Tchetche dakika ya 83.
Malik alifunga bao lake akiunganisha krosi maridadi ya beki wa kulia wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Erasto Nyoni, wakati raia wa Ivory Coast, Kipre Tchetche alifunga kwa penalti baada ya beki wa Mgambo, Ramadhan Kambwili kumuangusha Farid kwenye eneo la hatari.
Azam ingeweza kupata ushindi mnono zaidi kama si washambuliaji wake, Kipre na John Bocco kupoteza nafasi kadhaa nzuri za kufunga kwenye mchezo huo.
Kikosi cha Azam FC leo kilikuwa; Mwadini Ally, Erasto Nyoni, Waziri Salum, Said Mourad, Aggrey Morris, Kipre Balou, Brian Umony/Farid Malik, Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Humphrey Mieno/Khamis Mcha, John Bocco na Farid Malik.
Mgambo JKT; Tony Kavishe, Daud Salum, Salum Mlima, Bakari Mtama, Bashiru Chanacha, Novat Lufunga, Nassor Gumbo, Mohamed Samatta, Mohamed Netto, Salum Gilla na Peter Malyanzi.
Katika mechi nyingine, mabao ya Juma Luizio dakika ya nne na saba yameipa Mtibwa Sugar ushindi wa 2-1 dhidi ya JKT Ruvu ambayo bao lake lilifungwa na Salum Machaku dakika ya 52, Uwanja wa Manungu, Turiani, Morogoro.
JKT Oljoro imetoka sare ya 2-2 na Ruvu Shooting Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha, Mabao ya Oljoro yamefungwa na Nurdin Mohamed dakika ya 25 na Fikiri Mohamed dakika ya 64, wakati ya Ruvu yamefungwa na Elias Maguri dakika ya tatu na 40.
Mbeya City imeshinda ugenini, Uwanja wa Ally Hassan Mwinyi, Tabora mabao 3-1 dhidi ya wenyeji Rhino Rangers.
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BONGONEWS TZ - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger