Home » » AIBU YA MWAKA...!!! MKE WA MTU AFIA NYUMBANI KWA MWANAUME MWINGINE....

AIBU YA MWAKA...!!! MKE WA MTU AFIA NYUMBANI KWA MWANAUME MWINGINE....


Marehemu Elizabeth au mama Gerald enzi za uhai wake.

MWANAMKE aliyejulikana kwa jina moja la Elizabeth au mama Gerald amefia kwa mwanamme anayedaiwa kuwa naye ni mumewe ikiwa ni siku chache tangu atoke kwa mumewe wa ndoa, Risasi Mchanganyiko linaibumburua.

Mwanamke huyo alifariki dunia Ijumaa ya wiki iliyopita na kuzikwa Jumapili majira ya 10  jioni, Kawe jijini Dar es Salaam huku msiba huo ukigubikwa na utata kutokana na mazingira ya kifo cha mwanamke huyo.

KILIVYOSEMA CHANZO
Kwa mujibu wa chanzo cha habari, marehemu  Elizabeth alifunga ndoa na Emma Mtiku mwaka 2003 jijini Dar es Salaam na kufanikiwa kupata watoto wanne, wawili kwa sasa ni marehemu.

NDOA YAANZA KUINGILIWA
Mpashaji wetu anazidi kuweka wazi kwamba,  miaka tisa ya ndoa yao, amani, utulivu na upendo wa hali ya juu vilitawala lakini mwaka jana wakiwa uhamishoni Masasi mkoani Mtwara, shetani alihamishia majeshi yake kwenye ndoa hiyo.
Mwanaume ambaye marehemu Elizabeth alifia kwake.

MAMBO YALIANZIA HAPA
“Mwaka juzi mume wa Eliza alihamia Masasi,  akaenda na familia yake. Wakiwa huko, mwaka jana sasa, mwanamke huyo alikumbwa na ugonjwa mbaya. Alivimba mguu mmoja wa kushoto kama vile tende. Akakubaliana na mumewe yeye aje Dar ambako ni nyumbani kwa mama yake mdogo kwa ajili ya matibabu.
“Alikaa kwa muda nyumbani kwa mama’ke mdogo mpaka akapona huku akiendelea kutumia dawa za mitishamba, lakini uso wake ukawa hauoneshi dalili yoyote ya kurejea Masasi kuendelea na maisha ya ndoa na mumewe,” alisema mtoa habari hiyo.

NYUMA YA PAZIA
Taarifa ziliendelea kudai kuwa, wakati mwanamke huyo akiendelea ‘kubugia miti shamba’ nyumbani kwa mama yake mdogo jijini Dar, alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanamme mmoja aliyetajwa kwa jina moja la Mgima.
Ikasemekana muda mfupi baada ya kupona kabisa, Elizabeth aliamua kwenda kuishi kwa mwanamme huyo kwa siri huku mumewe Masasi akijua mke huyo anajiangalizia afya kwa mama yake mdogo! Jamani shetani huyu!

MAHARI MARA MBILI!
Inadaiwa kuwa mwanaume huyo mpya alijua Elizabeth ni mwanamke huru hasa baada ya kuwa naye kwa muda mrefu  bila kukutana na maisha yenye utata kutoka kwake, hasa kwenye simu.
“Mwishowe jamaa hakuona sababu ya kuendelea kuishi na mwanamke bila uhalali, akatangaza ndoa ambapo ilikuwa ifungwe mapema mwaka huu,” kilisema chanzo.
Kikaendelea: “Mipango ya ndoa ilianza, mahari ilipokelewa na yule mama mdogo wa Eliza.”

MUME WA MASASI AANZA KUCHEZWA NA MACHALE
Chako ni chako tu! Mtiku kule Masasi alianza kuingiwa na wasiwasi baada ya kuona mawasiliano yake na mkewe yanazorota siku hadi siku wakati alishatoa maagizo kwamba endapo kutakuwa na mabadailiko yoyote ya afya kwa mkewe ajulishwe ili hatua nyingine za kimatibabu zichukuliwe.

UPELELEZI WAANZA
Ilizidi kudaiwa kuwa, baada ya Mtiku kuzidiwa na wasiwasi juu ya mkewe aliamua kumtumia rafiki yake aishie Dar ampigie simu mkewe amwelekeze alipo huko mama mdogo ili akajue kinachoendelea.
Jitihada za rafiki huyo kukutana na shemeji yake zilikuwa zikigonga mwamba mara zote walipowasiliana kufuatia kupigwa danadana.

RAFIKI ATINGA UKWENI
Akiwa na uchungu wa ndoa ya rafikiye kuguswa na ‘kucha’ za shetani, swahibu huyo aliamua ‘kusaga lami’ hadi Kawe ili akamshuhudie shemejiye. Apofika aliambiwa alishapona lakini kwa siku hiyo alikwenda Kimara kuwapa ‘hai’ ndugu wengine.

MAJIRANI WABUMBURUA ISHU
Kifo cha nyani miti yote huteleza! Rafiki huyo akiwa anatoka nyumbani kwa mama mdogo wa marehemu, jirani mmoja (jina lake halikupatikana) alimvuta mkono na ‘kumng’ata’ sikio akidhani ndiye mume wa Elizabeth.
Alimwambia kuwa asijisumbue kwani mkewe anaishi na mwanamme mwingine na alishatolewa mahari, rafiki huyo akampigia simu Mkuti kumwelezea.

KUUGUA UPYA
Inaelezwa kuwa, mipango ya ndoa ikiwa inaendelea mwanzoni mwa mwezi ulioisha (wa tisa) Elizabeth alianza kuugua mwili mzima huku ule mguu nao ukianza kumsumbua kama awali.

MAUTI
Ibilisi alishikilia msimamo wake wa kuleta majanga kwa Eliza ambapo Ijumaa iliyopita alitangulia mbele ya haki palipo na makazi ya milele ya wanadamu.

ULINZI MSIBANI
Baada ya gazeti hili kutaarifiwa juu ya habari hizi, ‘wahangaikaji’ kupitia Oparesheni ya Fichua Maovu (OFM) iliweka kambi msibani hapo ambapo baada ya ndugu wa upande wa mwanamme huyo kusikia uwepo wa waandishi wetu, aliimarisha ulinzi ili wapigapicha wetu wasipate picha hata moja lakini kwa umakini wao walifanikiwa.

MWANAMME AZUNGUMZA
Baada ya sokomoko hilo, waandishi wetu walimtafuta mwanamme wa marehemu Eliza ambapo licha ya kukiri kuwa alijua Elizabeth aliwahi kuolewa ila hakuwa tayari kuzungumzia hayo kwa wakati huo kwa sababu bado alikuwa katika maumivu makali kwa wakati huo.
“Ni kweli Elizabeth alikuwa mke wa mtu, lakini habari hizi nilizipata hivi karibuni nikiwa katika kuumuliza, akaugua na hatimaye kifo. Nilipanga mwenzangu apone kwanza ndipo tujadiliane kuhusu hilo...inaniuma sana na kwa sasa naomba mniache,” alisema mwanamme huyo huku akiamka na kwenda sehemu nyingine.

MUME WA AWALI
Mume wa awali wa marehemu, Mtiku alipopatikana hewani kwa simu yake ya mkononi alithibitisha madai yote kuwa ni ya kweli na kwamba anachotaka kwa sasa ni pete ya ndoa na cheti cha kifo cha mkewe.
“Kweli mimi ndiye mume wa Eliza, yote hayo ni kweli. Kwa sasa sina la kusema ila ninachotaka ni pete na cheti cha kifo.
“Sisi Wakatoliki mke akifa hazikwi na pete, mume anaivaa kwenye kidole chake zinakuwa mbili ili watu wajue ni mjane,” alisema mume huyo
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BONGONEWS TZ - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger