Home » , » YANGA YAUA KAGERA, SHUJAA NGASSA NA KIIZA, SIMBA SC YAENDELEA KUNG'ARA KILELENI ...

YANGA YAUA KAGERA, SHUJAA NGASSA NA KIIZA, SIMBA SC YAENDELEA KUNG'ARA KILELENI ...

  SIMBA SC jioni hii imezidi kupaa kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Prisons ya Mbeya kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Bao pekee la Simba SC katika mchezo huo limefungwa na kiungo Jonas Mkude dakika ya 62 na sasa Wekundu hao wa Msimbazi wanatimiza pointi 18 baada ya kucheza mechi nane.   

Jonas Mkude

Simba SC inatarajiwa kuingia kambini kujiandaa na mchezo dhidi ya wapinzani wao wa jadi, Yanga SC Oktoba 20, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam baada ya mechi ya leo.
Uwanja wa Kaitaba, mabingwa watetezi Yanga SC wamepata ushindi wa kwanza ugenini msimu huu baada ya kuilaza Kagera Sugar mabao 2-1, hivyo kupaa hadi nafasi ya pili kwa kufikisha pointi 15.
Yanga SC walikuwa wa kwanza kupata bao dakika ya pili mfungaji Mrisho Ngassa aliyeunganisha kwa kichwa mpira wa kurushwa wa beki wa kulia Mbuyu Twite.
Baada ya bao hilo, Yanga walicharuka kusaka mabao zaidi, lakini Kagera Sugar walisimama imara na kujizuia kuruhusu mabao zaidi.
Hadi mapumziko, Yanga walikua mbele kwa bao hilo 1-0, lakini dakika ya pili tu baada ya kuanza kipindi cha pili, mshambuliaji Godfrey Wambura aliisawazishia Kagera baada ya kuuwahi mpira uliozuiliwa na mabeki wa Yanga kufuatia krosi maridadi ya Paul Ngway.
Yanga walicharuka baada ya bao hilo na kuzidisha mashambulizi langoni mwa Kagera, hatimaye kufanikiwa kupata bao la ushindi dakika ya 59 mfungaji Hamisi Kiiza ambaye alimtoka beki Ernest Mwalupani baada ya kupigiwa pasi ndefu na Mbuyu Twite.      
Baada ya bao hilo, kasi ya mchezo iliongezeka kwa pande zote mbili, Kagera wakisaka bao la kusawazisha na Yanga wakitaka mabao zaidi, lakini hadi refa Hamad Kikumbo wa Dodoma anapuliza kipyenga cha kuhitimisha mchezo huo, matokeo yalibaki 2-1.
Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite, David Luhende, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Athumani Iddi ‘Chuji’, Mrisho Ngassa, Frank Domayo, Didier Kavumbangu, Hamisi Kiiza/Hussein Javu dk89 na Haruna Niyonzima/Simon Msuva dk60.   
Kagera Sugar; Agathon Anthony, Benjamin Asukile, Salum Kanoni, Maregesi Mwangwa, Ernest Mwalupani, George Kavilla/Rashid Roshwa dk78, Godfrey Wambura, Daudi Jumanne, Themi Felix, Suleiman Kibuta na Paul Ngway/Bukenya Kitagenda dk67.
Ngassa akishangilia na Mbuyu Twite baada ya kufunga
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BONGONEWS TZ - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger