Home » » WATUHUMIWA WA KESI YA UNYANG'ANYI WA KUTUMIA SILAHA NA KULICHOMA MOTO KANISA LA KKKT USHARIKA WA MBAGALA WAACHIWA HURU...

WATUHUMIWA WA KESI YA UNYANG'ANYI WA KUTUMIA SILAHA NA KULICHOMA MOTO KANISA LA KKKT USHARIKA WA MBAGALA WAACHIWA HURU...


Mahakama ya Hakimu mkazi Kisutu Dar es salaam, imewaachiria huru Hamed Sekondo na wenzie nane walikuwa wakikabiliwa na kesi ya unyang'ang'anyi wa kutumia silaha na kisha kulichoma moto Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Mbagala, baada ya kuwaona hawana kesi ya kujibu.

Uamuzi huo wa kesi hiyo ya jinai namba 294/2012 umetolewa na Hakimu Mkazi, Waliarwande Lema.

Hakimu Lema alisema, “upande wa Jamhuri katika kutaka kuthibitisha kesi yao uliweza kuleta jumla ya mashahidi 14 wakati awali kesi hiyo wakati inafunguliwa mahakamani hapo mwaka jana ilikuwaa jumla ya washitakiwa 10.”

Hivi karibuni mshitakiwa mmoja aitwaye Ramadhani Mbulu alifariki dunia na hivyo kufanya kesi hiyo kubakiwa na washitakiwa 9. Watuhumiwa kwa kipindi chote hicho walikuwa wakiishi gerezani kwa kosa la unyang'anyi wa kutumia silaha lililokuwa likiwakabili lilikuwa halina dhamana. Washitakiwa hao walikuwa wakitetewa na wakili wa kujitegemea Yahya Njama.

'Baada ya kusikiliza na kuchambua ushahidi na vielelezo vilivyotolewa na upande wa Jamhuri, mahakama hii imefika uamuzi wa kuwaona washitakiwa wote hawana kesi ya kujibu chini ya kifungu cha 230 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, hivyo inawaachiria huru kwa sababu upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha kesi yao. Ushahidi wote walioutoa ni dhahifu na imeshindwa kishawishi Mahakama iwaone washitakiwa wana kesi ya kujibu,” alisema hakimu Lema.

Upande wa Jamhuri uliwakilishwa na wakili mwandamizi Tumain Kweka, Inspekta wa polisi Hamis Said.

Mwaka jana katika eneo la Mbagala jijini Dar es Salaam lilikumbwa na vurugu kubwa zilisosababisha Kanisa kuchomwa moto, na walioripotiwa kuwa ni baadhi ya waumini wa Kiislamu wakipinga dini yao kudhalilishwa kutokana na madai kuwa kijana mmoja alikikojolea kitabu Kitakatifu cha imani yao, yaani Quran.

--- Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Oktoba 18 mwaka 2013
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BONGONEWS TZ - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger